KILICHOMUONDOA TAMBWE HIKI HAPA, PHIRI ANENA.

12/21/2014 09:12:00 pm
Kocha wa Simba Patric Phiri Akitoa maelekezo kwa wachezaji wake.
KWA mara ya kwanza, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri, amefunguka na kueleza kilichosababisha Amissi Tambwe akose nafasi kwenye kikosi chake, kwa kile alichosema hakuwa na uwezo wa kupambana na mabeki wenye nguvu ukimlinganisha na Elias Maguli.

Kauli ya Phiri imekuja siku chache baada ya Tambwe kusitishiwa mkataba wake Msimbazi, akidaiwa kushuka kiwango wakati alifanya  vyema enzi za Mcroatia, Zdravko Logarusic na Abdallah Kibadeni, hadi kufanikiwa kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Phiri alisema kuwa Tambwe ni mchezaji mzuri, lakini kilichomfanya asiwe na furaha Simba ni kukaa benchi, hivyo kuvurugika kisaikolojia na kujikuta akishindwa kutimiza majukumu yake kwa ufanisi akiwa uwanjani.

“Ukiangalia nilikuwa nikimpanga Maguli katika mechi ambazo niliamini zina mabeki wagumu kupitika, kitu ambacho Tambwe hakuweza kufanya, lakini alikuwa mzuri katika mechi zisizo na beki ngumu.

“Jambo hilo lilimfanya apoteze kujiamini na kukosa nafasi, hivyo kuathirika kisaikolojia na kujikuta akishindwa kufanya vizuri ndani ya uwanja,” alisema Phiri.

0 comments:

Post a Comment